Quantcast
Channel: MAFUNDISHO – Strictly Gospel
Viewing all articles
Browse latest Browse all 46

Jiweke sawa katika utumishi wako 2013!!

$
0
0

pastor

MUNGU ANAPOKUMBUKA

Naomba sasa tufunguwe kwa pamoja katika kitabu cha Isaya 43:26, Biblia inasema “Unikumbushe, na tuhojiane; eleza mambo yako, upate kupewa haki yako”.

Mstari tuliousoma unaonyesha kana kwamba kuna tatizo katika kumbukumbu ya Mungu ndiyo maana anahitaji akumbushwe. Labda utaniuliza kwani huyo anayesema unikumbushe ni Mungu? Je, unaweza kuthibitisha kuwa ni Mungu? Ukisoma kuanzia mstari wa kumi na tano wa sura hii utaona kuwa anayesema maneno haya ni Mungu mwenyewe.

Kabla sijaendelea na kuuchambua mstari huu, naomba turudi kwenye ujumbe wa somo letu; MUNGU ANAPOKUMBUKA. Mpendwa, Mungu anapokumbuka ni lazima kitu cha tofauti kitokee, jambo la tofauti litokee, matumaini yarejeshwe, Baraka zimiminike, ushindi upatikane ….. kwa sababu Mungu amekumbuka. Wakati huu ulionao tamani sana Mungu akukumbuke, maana mambo hubadilika sana Mungu anapomkumbuka mtu, maombi hujibiwa na muujiza hutokea.

Hebu utuangalie baadhi ya mifano katika Biblia inayoonesha Mungu alipokumbuka nini kilitokea……. Alipomkumbuka Nuhu (nyakati zile za gharika – Mwanzo 8:1) alivumisha upepo na Nuhu, mkewe, wanawe na wakwe zake pamoja na kila chenye uhai wakatoka katika safina. KUTOKA KWA NUHU KATIKA SAFINA KULIHITAJI MUNGU AKUMBUKE!

Alipomkumbumbuka Ibrahimu (wakati wa Sodoma na Gomora), Mungu alimtoa Lutu asiangamie katika miji ile (Mwazo 19:29). Kumbe Lutu aliepuka kuangamia baada ya Mungu kumkumbuka Ibrahimu.

Alipolikumbuka agano lake alilolifanya na Ibrahimu, Isaka na Yakobo, aliwatoa wana wa Israel katika utumwa wa Msri (Kutoka 2:24 na 6:5).  Bwana alipomkumbuka Hanna, mwanamke huyu aliyeonekana hawezi kuzaa alichukuwa mimba akamzaa mwana akamwita Samwel (1Samwel 1:11, 19-20).

Mungu alipokumbuka sadaka na maombi ya Kornelio alimtuma Petro ili kupeleka wokovu kwa Mataifa. Kumbuka kuwa Petro alikuwa ni  muumini mkubwa wa uyahudi asiyetaka kuchamana na mataifa (Matendo 10:4), Dorkasi anafufuliwa kwa sababu ya kumbukumbu ya kuwahudumia wajane (Matendo 9:36-39) na kupitia kufufuliwa huko watu wengi wakamwamini Yesu katika mji wa Yafa.

Najua kuna watu wengi sana ambao Mungu aliwakumbuka kisha jambo la tofauti likatokea katika maisha yao. Lakini naomba nimalizie ujumbe wangu kwa kuwaelezea watu wawili ambao Mungu aliwakumbuka. Pia nitakuwa najibu swali nililoulizwa mwanzo mwa ujumbe wangu,

Hata hivyo napenda uzingatie hiki KUMBE MUNGU AKIKUMBUKA KUNA KITU CHA TOFAUTI HUTOKEA. Haijalishi uko katika hali gani inayokatisha tamaa, usihangaike mpendwa mfanye Mungu akukumbuke. Hebu tuangalie mifano ya watu hao wawili. Mmoja kutoka Agano la Kale na wa pili kutoka Agano jipya.

Ukisoma katika Kitabu cha Isaya 48:1 – 8, utaona habari ya mfalme Hezekia, ambaye muda wake wa kuishi katika dunia hii ulikuwa umefikia mwisho. Nabii wa wakati huo, Isaya alitumwa kupeleka habari kuwaatengeneze mambo ya nyumba yake maana HAKIKA ATAKUFA – Mstari wa 1. Hezekia hakuanza kupishana na Nabii Isaya. Badala yake aligeukia ukutani  akamwomba Mungu.

Hebu angalia vizuri mstari ule wa 3, “akasema, Ee Bwana, KUMBUKA HAYA, nakusihi,,,,,,,,,,”, Hezekia hakulalamika bali alimkumbusha Mungu yale aliyoyatenda katika kipindi cha ufalme wake. Kama ungependa kujua alichokifanya mfalme Hezekia,  kwa wakati wako soma 2Wafalme 18:1 – 7. Kwa sababu alijua amemfanyia nini Bwana alikuwa na ujasiri wa kumwambia Bwana KUMBUKA.

Sote tunajua kuwa unabii ambao ulinenwa kwa Hezekia kuwa HAKIKA ATAKUFA ulibatilishwa, Hezekia akaongezea miaka 15 na ishara ikafanywa, kwa sabu Mungu amemkumbuka mtumishi wake Hezekia.

KUUUMBE, Mambo tunayoyafanya kwa ajili ya Bwana ni hazina!!! Na kwa hayo unaweza kuyatumia Kumkumbusha Bwana! Kumbe Mungu hana tatizo la kumbukumbu isipokuwa anataka uhojiane naye (u-present case yako) umweleze mambo uliyoyafanya kwa ajili ya utukufu wa jina lake, utoe sababu ya kupata/kuongezewa hicho unachokitaka … Mpendwa hebu jihoji mwenye, je, unacho cha kumwambia Mungu akumbuke ambacho umekifanya kwa ajili yake na kwa utukufu wake? Ulikifanyaje?

Mpendwa naomba uliangalie tukio la Hezekia kwa utazamo huu, Hezekia alipokuwa mfalme,,, Mungu alimtarajia afanye mambo kadha wa kadha, Hezekia katika nafasi yake alifanya mambo mengi kwa ajili ya Mungu. Tatizo lilipokuja katika maisha yake na likaonekana kuwa ni lazima aondoke na mjumbe akatumwa kwake, Hezekia ali-appeal kwa kutumia mambo aliyomfanyia Bwana. Hakupeleka hoja kuwa Mungu give me another chance, this time ninaahidi nitafanya moja mbili tatu. Bali yeye alimtaka Mungu wake akumbuke yale aliyoyafanya.

Sasa naomba ujihoji mpendwa katika nafasi uliyopo/uliyonayo kuna mambo yo yote unayoyafanya kwa ajili ya Bwana ili jina lake litukuzwe. Ama unasubiri ukibanwa na shida/adha/majaribu ya kutisha ndipo umuahidi Mungu utakayoyafanya.katika mwili wa Kristo je umefanya nini kwa ajili ya Bwana?

Mtu wa pili ambaye ningependa tuangalie habari zake ni yule mwizi msalabani ambaye alisulubiwa pamoja na Bwana wetu Yesu (Luka 23:39 – 43). Biblia inaonyesha kuwa Bwana Yesu aliposulubiwa wezi wawili walisulubiwa pamoja naye. Mwizi aliyekuwa upande mmoja alianza kumdhihaki Bwana Yesu. Ndipo yule mwizi aliyekuwa upande mwinge akamkemea na kumdhibiti kabisa mwizi mwenzie. Ni rahisi kwa mwizi kumdhibiti mwizi mwenzie.  Baada ya kuhakikisha kuwa umemdhibiti mwizi mwenzake alimgeukia Bwana Yesu na kumwambia ….”Ee Yesu, nikumbuke utakapoingia katika ufalme wako”. (mstari wa  42).

Mwizi huyu alipofanya kazi ya kumkemea na kumnyamazisha mwizi mwenziwe, alipata kisemeo  mbele za Bwana na kuleta hoja ya kukumbukwa. Alipomfanyia Mungu kazi aliomba akumbukwe. Na bila kuchelewa Yesu alimwambia hivi …….“leo hivi utakuwa pamoja nami peponi”. (mstari 43).

Watu wote niliyowataja hapo juu wanafanana kwa kitu kimoja walikifanya jambo kwa ajili ya Mungu ndipo Mungu akawakumbuka. Hata (mfalme Hezekia na mwizi msalabani)  mmoja katika nafasi ya mfalme na mwingine akiwa msalabani, walifanya kitu mbele za Mungu na kuomba Mungu awakumbuke. ELEWA HIVI hali uliyonayo (iwe ikulu au msalabani) sio kigezo cha kushindwa kufanya kazi ya Mungu ili jina lake litukuzwe!!!

Sasa naomba nimalizie ujumbe huu kwa kusema maneno haya; lengo la ujumbe huu nilitaka kumtia moyo mtu ambaye anamfanyia Mungu kazi katika eneo lo lote alipo, kuwa kazi yako si bure. Biblia inasema “………mkazidi sana kutenda kazi ya Bwana sikuzote, kwa kuwa mwajua ya kwamba taabu yenu siyo bure katika Bwana.” – 1Korintho 15:58.

Kama taabu yetu si bure basi ina malipo/ujira. Bwana wetu anasema … “Tazama, naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo.” – Ufunuo 22:12. Swali ni kwamba, Je, kazi unayoifanya inastahili malipo, inakidhi viwango vya mbinguni? Mungu akikuangalia anaona unafanya kazi yake kwa ajili yake? Hebu angalia unapofanya kazi ya Mungu unafanyaje. Je, unatimiza wajibu, unafanya kwa mazoea, kwa manung’uniko, malalamiko, kwanini nyingi  na masikitiko kadha wa kadha. BASI WAPENDWA TUJIANGALIE SANA TUNAVYOFANYA UTUMISHI WETU MBELE ZAKE……………. MUNGU YUPO TAYARI KUTUKUMBUKA.

Hivyo unapojiandaa kuupokea mwaka 2013, jiweke sawa katika utumishi wako, ili uwe ni mwaka wa kuweka akiba/hazina ya utumishi mbele za Mungu aliye tayari kukumbuka yote uliyoyafanya kwa ajili yake na kubadilisha hali yako. Kazi kwako mtumishi wa Mungu.

Mshirika mpya SG.

Mathew.


Filed under: MADHABAHUNI, MAFUNDISHO

Viewing all articles
Browse latest Browse all 46

Trending Articles